RSS
Iran ni kinara wa mwamko, umoja na heshima ya mataifa ya Kiislamu (2010/07/10 - 21:36)

Ayatullah Khamenei amewapongeza Waislamu wote kwa mnasaba wa siku ya leo ya kukumbuka tukio la kupewa utume Mtume wetu Muhammad (saw) na akaongeza kuwa kutokana na kufungua njia za uadilifu, amani, usalama na utulivu, tukio hilo limetambuliwa kuwa ni rehma ya Mwenyezi Mungu. Ameongeza kuwa njia hizo za utulivu na amani zinaanzia ndani ya roho ya mwanadamu hadi katika jamii na dunia nzima na wale wanaotambulishwa na Uislamu kuwa ni wapinzani wa njia hizo za uongofu ni watu na makundi yanayopinga saada na ufanisi halisi wa mwanadamu.

Huku akisoma aya za Qur'ani Tukufu na kuashiria mwenendo wa Mtume unaowataka Waislamu kukabiliana na watu wanaopinga saada na ufanisi wa mwanadamu, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema: "Uislamu umetumia hoja za wazi katika kuwalingania wanadamu wote maisha ya saada na ufanisi chini ya kivuli cha amani, uadilifu na usalama, na wakati huo huo umetoa amri ya kukabiliana vilivyo na watu wanaoweka vizuizi katika njia hiyo."

Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema, katika kipindi chote cha historia wapinzani wa njia yenye nuru ya saada na ufanisi wa mwanadamu wamekuwa wakianzisha vita mbalimbali si kwa ajili ya kueneza uadilifu na amani bali kwa shabaha ya kupanua mamlaka yao, kueneza dhulma na kuvuruga amani na utulivu wa wanadamu. Ameongeza kwamba hii leo pia madola makubwa ya kibeberu yanadumisha njia hiyo hiyo ya kijahilia lakini kwa kutumia teknolojia na silaha za kisasa zikiwemo za nyuklia.

Ayatullah Khamenei amesema kuwa silaha za madola makubwa ya kibeberu na gharama kubwa zinazotumiwa kununulia silaha hizo ni miongoni mwa masuala yanayosikitisha ya dunia ya sasa. Amesema kuwa maadamu madola makubwa yanaendelea kuongoza masuala ya dunia, basi vita, ukosefu wa amani na dhulma vitaendelea kushuhudiwa.

Akibainisha kuwa katika kipindi chote cha miaka 45 ya baada ya kumalizika Vita vya Pili vya Dunia hadi mwaka 1990 kumekuwepo vita dunia isipokua katika kipindi cha wiki tatu tu, Ayatullah Khamenei amesema vita hivyo vinaanzishwa na nchi zinazoshika nafasi za kwanza katika kutengeneza silaha kwa wingi duniani na zinataka kupata faida kutokana na kuuza zana za kijeshi. Amesisitiza kuwa madai ya Marekani kwamba inaanzisha vita kwa ajili ya kuimarisha amani na uadilifu ni urongo mtupu.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria takwimu rasmi za gharama za kununulia silaha za Marekani ambazo zimefikia dola bilioni 600 katika mwaka uliopita na akasema: "Zana hizo za kivita zinatumiwa kwa shabaha ya kulikandamiza taifa la Waislamu wa Afghanistan, kulidhibiti zaidi taifa la Iraq na kuusaidia utawala habithi wa Kizayuni wa Israel kwa ajili ya kuendeleza ghasia na machauko katika eneo la Mashariki ya Kati.  

Amesema inasikitisha kwamba mfumo huo wa kidhalimu na kijahili ndio unaotawala dunia na maisha ya watu lakini kwa kuwa mwenendo huo ni kinyume na kanuni za Mwenyezi Mungu katika maumbile na kinyume na haki hapana budi utatoweka na dalili za kuangamia kwake zimeanza kudhihiri.

Ayatullah Ali Khamenei ameashiria mabadiliko ya hali ya dunia ya sasa na mwamko unaoshika kasi zaidi wa ulimwengu wa Kiislamu na akasema: "Moja ya sababu za kuanza kutoweka madola ya kibeberu ni mwamko wa Kiislamu wa Waislamu ambao umeyafanya madola hayo yapoteze nguzu na uwezo wao; suala ambalo linathibitishwa na hali ya sasa ya Marekani ikilinganishwa na miaka ya huko nyuma.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza juu ya udharura wa kuimarishwa zaidi umoja na mshikamano kati ya Waislamu na akasema: "Wapinzani wa njia ya tauhidi na ufanisi wa mwanadamu wanahisi hatari kubwa mahala popote panapokuwa na mwamko zaidi wa Kiislamu na ni kwa sababu hiyo ndiyo maana uadui dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu umekithiri zaidi.

Ayatullah Khamenei amesema kuwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni kinara wa mwamko, umoja na heshima ya mataifa ya Kiislamu. Amesema ni miaka 31 sasa ambapo madola ya kibeberu yanafanya njama dhidi ya mfumo wa Kiislamu hapa nchini lakini licha ya uadui huo Jamhuri ya Kiislamu imepata nguvu kubwa na kuwa imara zaidi kuliko huko nyuma.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa mwenendo huo utaendelea na kwamba ahadi ya kweli ya Mwenyezi Mungu ni kutoweka na kuangamia batili. Ameongeza kuwa kadiri kiwango cha uhasama kinavyoongezeka ndivyo wananchi katika ulimwengu wa Kiislamu wanavyozinduka zaidi. Amezitaka serikali na mataifa ya Kiislamu kujiamini zaidi na kutoyaogopa madola ya kibeberu kwani nguvu zao ni bandia, zisizokuwa halisi na zinazotoweka.

Mwanzoni mwa mkutano huo Rais Mahmoud Ahmadinejad amewapongeza Waislamu kwa mnaba wa kuadhimisha siku ya kubaathiwa na kupewa utume Nabii Muhammad (saw) na akasema kuwa lengo na hakika na tukio hilo ni kulingania watu dini inayooana na maumbile halisi ya mwanadamu na kumuokoa kiumbe huyo. Dakta Ahmadinejad amesema ujumbe wa tukio la kupewa utume Mtume wa Uislamu ni kuwafanya watu waja wa kweli wa Mola Muumba, neno la tauhidi na kumpwekesha Mwenyezi Mungu, kueneza uadilifu na kukabiliana na watawala madhalimu na mashetani, mambo ambayo matokeo yake ni saada na ufanisi wa mwanadamu.

Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ameashiria woga na wahaka unaoongezeka kila siku wa madola ya kishetani kutokana na mwamko wa wanadamu na akasema: "Kama ambavyo Mwenyezi Mungu Mtukufu alivyoahidi, ardhi hii watarithi watu wema, na matunda ya kubaathiwa Mtume wa Uislamu yatadhihiri chini ya uongozi wa mwanae Imam Mahdi (as)."