RSS
Harufu ya marashi ya Mapinduzi ya Kiislamu imezitia nishati nyoyo za mataifa mbalimbali (2010/07/14 - 18:02)

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Ali Khamenei mapema leo siku moja kabla ya maadhimisho ya tarehe tatu Shaabani inayosadifiana na siku aliyozaliwa Bwana wa Mashahidi Imam Hussein (as) amehutubia maelfu ya makamanda wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (Sepah) akisema kuwa masuala ya kiroho na kimanawi yanayotawala katika jeshi hilo ndiyo sababu ya utendaji kazi mzuri wa taasisi hiyo ya wananchi na ya kimapinduzi katika nyanja mbalimbali na mazingira tofauti ya kipindi cha miongo mitatu iliyopita. Ayatullah Khamenei amebainisha masuala muhimu ya ndani na ya kimataifa na akasisitiza kuwa viongozi wote wa nchi hii wanapaswa kutekeleza majukumu yao mazito katika medani mbalimbali na kujitayarisha kwa ajili ya kukabiliana na kila jambo kama ilivyokuwa katika kipindi chote cha miaka thalathini na moja iliyopita. Amesema kuwa hapana shaka taifa kubwa la Iran na Jamhuri ya Kiislamu itaibuka mshindi katika mpambano huo kama ilivyokuwa huko nyuma.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameutaja mwezi wa Shaaban kuwa ni mwezi wa dhikri, kuomba na kuijenga upya nafsi. Ametoa mkono wa baraka na pongezi kwa minasaba ya mwezi huu wa Shaaban ambayo ni kuzaliwa Imam Hussein, Imam Sajjad na Abul Fadhl al Abbas (as) na akasema kuwa jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ni jeshi la wafuasi wa kweli na wapenzi wa njia ya Mwenyezi Mungu na Maimamu wa njia ya uongofu.

Akifafanua muundo wa kiroho na wa ndani wa jeshi la Sepah, Ayatullah Khamenei amesema: "Nyoyo zenye hamu kubwa ya kupigana katika njia ya Mwenyezi Mungu katika medani zote, kusema ukweli na kuona na kuitambua haki ni mambo matatu yanayounda utambulisho halisi wa jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu."

Akiashiria vipengee vya dua tukufu ya mwezi wa Shaaban, Amirijeshi Mkuu wa majeshi ya Iran amesema kuwa vuguvugu na shauku kubwa inazikurubisha nyoyo za wanasepah kwa Mwenyezi Mungu na ukweli na ikhlasi yao katika nia, maneno na matendo inawainua juu na kuwaelekeza kwa Mola Mtukufu, kama lilivyo neno zuri.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amekutaja kuona na kutambua haki kuwa ni miongoni mwa nguzo tatu za utambulisho halisi wa jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu. Amesema sifa hiyo inaliwezesha jeshi la Sepah kuelewa uhakika wa mambo katika mazingira yote hata katika machafuko na hali ya kivumbi na ya kutatanisha.

Amirijeshi Mkuu wa majeshi ya Iran ameashiria historia ya kuasisiwa jeshi la Sepah na kusema kuwa jeshi hilo lilianzia ndani ya misikiti, shule, vyuo vikuu, nyumba na nyoyo za wananchi wenye imani kubwa. Ameongeza kuwa hakuna mtu aliyeunda jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu, bali jeshi hilo lilijitokeza lenyewe kulingana na mahitaji ya zama na lilikidhi mahitaji ya Mapinduzi ya Kiislamu na taifa mahala popote lilipohitajika.

Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa miongoni mwa sifa kuu za jeshi la Sepah ni kulinda utambulisho wake halisi na kutenda kazi kwa mujibu wa mahitaji ya zama na wakati. Amesisitiza kuwa jeshi hilo limeweza kulinda utambulisho wake katika miaka ya awali ya Mapinduzi ya Kiislamu, katika kupambana na maadui wa Mapinduzi kwenye mitaa ya Tehran, katika masuala ya mikoa ya mpakani, katika kipindi cha vita vya miaka 8 ya kujitetea kutakatifu na katika nyanja nyingine nyingi, kwenda na wakati na kutekeleza vyema majukumu yake.

Akiashiria wito wa viongozi wa wakati huo wa kulitaka jeshi la Sepah kuingia katika medani za ujenzi na ustawi wa nchi baada ya vita, Ayatullah Khamenei amesema kuwa katika medani hiyo pia Sepah ilichukua hatua bora zaidi mahala popote ilipoingia, suala ambalo linaonesha kwamba taasisi hiyo ya wananchi inakwenda ya wakati na kukamilika zaidi kadiri siku zinavyopita.

Amesema kuwa suala la kuanzishwa taasisi mbalimbali ikiwa ni pamoja na jeshi la Sepah na Jihadi ya Ujenzi ni miongoni mwa ubunifu na kazi kubwa za Mapinduzi ya Kiislamu hapa nchini. Ameongeza kuwa taasisi hiyo ina muundo unaokwenda na wakati sambamba na kulinda thamani na malengo yake; masuala ambayo yameiepusha na matatizo yanayozikumba taasisi nyingine kama hiyo.

Amirijeshi Mkuu wa majeshi ya Iran amesisitiza juu ya udharura wa kulindwa utambulisho halisi wa jeshi la Sepah na akasema kuwa taasisi hiyo ni mti uliobarikiwa ambao kwa mujibu wa Qur'ani Tukufu hutoa matunda makhsusi katika kila kipindi na zama. Amesisitiza kuwa sifa hiyo nzuri inapaswa kudumishwa.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa sharti la kuweza kubuni mipango sahihi kwa ajili ya harakati ya kufanikisha malengo ya Sepah ni kutambua uhakika wa hali ya sasa, kufanya uchunguzi na kutabiri hali ya baadaye. Ameashiria wajibu na kazi za makamanda wa jeshi hilo na Sepah kwa ujumla katika medani hiyo na akasema: "Kulinda utambulisho halisi wa masuala ya kiroho wa Sepah kunaliwezesha jeshi hilo kutambua uhakika wa mambo na kutabiri matukio ya siku za usoni." Ameongeza kuwa maarifa na utambuzi huo vinatayarisha uwanja mzuri wa kubuni na kuchukua hatua sahihi.

Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu ameendelea kujadili kadhia hiyo kwa kubainisha hali ya sasa hapa nchini na katika nyanja za kimataifa. Suala la kwanza ambalo Kiongozi Muadhamu ameliashiria ni uimara wa Mapinduzi ya Kiislamu hapa nchini.

Ili kuweza kuweka wazi uhakika huo, Ayatullah Khamenei amefanya ulinganisho baina ya Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran na mapinduzi ya Ufaransa na awamu zake mbalimbali zinazokinzana kikamilifu katika miongo yake ya mwanzoni. Amesema: "Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran, tofauti na harakati nyingine za kisiasa na kijamii za karne hii, yangali yanapiga hatua katika njia iliyowekwa na Uislamu baada ya kupita miaka 31 ya misukosuko mingi na Imam Khomeini akaweka njia zake za reli; jambo hili muhimu sana ni dalili ya himaya na msaada wa Mwenyezi Mungu kwa mapinduzi hayo."

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria pia matamshi ya viongozi wa Marekani kuhusu juhudi zinazofanywa na nchi hiyo kwa ajili ya kubadilisha mwenendo wa Iran na akasema kuwa maana halisi ya matamshi hayo ni njama za kubadili njia ya harakati ya Mapinduzi ya Kiislamu.

Ayatullah Khamenei amesema kuwa nyoyo zenye imani za taifa la Iran ni dhihirisho la kudura za Mwenyezi Mungu. Amesisitiza kuwa suala lililobakisha harakati ya Mapinduzi ya Kiislamu katika njia yake ya asili ni mapenzi ya taifa la Iran kwa Uislamu ambao umetengeneza ngome kubwa na isiyopenyeka kwa ajili ya Mapinduzi ya Kiislamu na nchi hii; na iwapo njia hiyo itabadilika na Uislamu kutoweka, ngome hiyo pia itasambaratika na kuruhusu madhalimu wavamizi kuingia nchini Iran.

Uhakika wa pili ulioashiriwa na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu kuhusu hali ya ndani ni maendeleo makubwa ya taifa hili. Amesema kuwa kwa mujibu wa takwimu za kimataifa, kasi ya maendeleo na kukua elimu na sayansi nchini Iran imeongezeka mara kadhaa ikilinganishwa na kiwango cha wastani duniani. Hata hivyo amekumbusha kuwa bado kuna masafa marefu hadi kufikia daraja za juu za elimu na sayansi ingawa kasi ya sasa haipaswi kufumbiwa macho.

Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amekutaja kuiva na kukomaa kisiasa wananchi wa Iran kuwa ni miongoni mwa uhakika usioweza kupingwa. Ameongeza kuwa wananchi, vijana na mabarobaro wamepata tajiriba na uzoefu mzuri kutokana na matukio mbalimbali ya kisiasa na wanaelewa vyema mambo kwa kadiri kwamba hata pale wanaposhawishika katika suala fulani la kutatanisha hubadilisha mwelekeo haraka na kurejea baada ya kutambua ukweli wa mambo. Amesisitiza kuwa ukweli huo umeshuhudiwa vyema katika fitina za baada ya uchaguzi wa Rais wa mwaka jana.

Ayatullah Ali Khamenei amesema kuwapo dini katika maisha ya vijana hapa nchini ni uhakika mwingine muhimu mno. Amesema kuwa mahudhurio makubwa ya vijana katika ibada ya itikafu, swala za jamaa katika vyuo vikuu na maeneo mengine na kushiriki kwao katika vikao vya kidini ni ithibati ya ukweli huo.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu pia ameashiria suala la kuenea fikra za Mapinduzi ya Kiislamu ulimwenguni. Amesema kuwa maana halisi ya kupeleka nje Mapinduzi ya Kiislamu ni kupeleka nje marashi na harufu nzuri ya fikra na malengo ya mapinduzi hayo. Ameashiria pia jinsi watu katika nchi mbalimbali wanavyowapokea kwa shangwe na furaha kubwa viongozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na akasema: "Harufu nzuri ya marashi ya Mapinduzi ya Kiislamu imezitia nishati kubwa nyoyo za mataifa mbalimbali, na huu ni ukweli ambao hauwezi kukanushwa."

Ayatullah Khamenei amezungumzia pia harakati inayoendelea ya kambi ya maadui wa Mapinduzi ya Kiislamu. Ameashiria njama zisizosimama lakini zilizofeli za utawala ghasibu wa Israel na Marekani kwa ajili ya kukabiliana na harakati kubwa ya taifa la Kiislamu la Iran na akasema: "Mapinduzi ya Kiislamu yameiondoa Iran adhimu na yenye nafasi ya kistratijia na maslahi mengi katika makucha ya Marekani na kukunjua jamvi la udhalili kwa ajili ya madhalimu wa kimataifa; kwa msingi huo madhalimu hao wamekuwa wakifanya uadui na njama katika miaka yote iliyopita dhidi ya taifa la Iran."

Ayatullah Khamenei ameifananisha Marekani na dhalimu mbabe anayewapokonya watu mali zao katika upeo wa kimataifa lakini hali yake inakuwa mbaya siku baada ya siku. Amesema baadhi ya wanatoa hongo kwa dhalimu huyo wa kimataifa kwa ajili ya kulinda biashara zao na wengine wenye nguvu kiasi wamekuwa wanafunzi wa kisiasa na kijeshi wa Marekani kutokana na kuchelea kukabiliana naye. Amesema baadhi ya wengine wanasimama kukabiliana na dhalimu huyo na kwamba Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imekuwa mstari wa mbele katika mapambano hayo kutokana na kusimama kidete kwa wananchi na viongozi wake.

Akiendelea kufafanua mwenendo unaokuwa kwa kasi wa kuichukia Marekani kati ya mataifa mbalimbali duniani, Ayatullah Khamenei ameashiria madai ya nchi hiyo baada ya kusambaratika Urusi ya zamani na kambi ya Mashariki na akasema wakati huo serikali ya Marekani ilitoa fikra na mfumo mpya wa kimataifa chini ya uongozi wa White House lakini hii leo viongozi wa nchi hiyo wanakabiliwa na maandamano na upinzani unaozidi kila siku wa watu katika pembe mbalimbali za dunia, na chuki na uadui huo wa watu dhidi ya Marekani haupungui licha ya juhudi kubwa zinazofanywa na viongozi wa Washington.

Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria pia kufeli kwa siasa za Marekani huko Iraq, Afghanistan, Lebanon na Palestina na akasema: "Licha ya madai yake yote, Marekani na utawala wa Kizayuni wa Israel zimeshindwa kuiondoa madarakani serikali ya harakati ya Hamas katika Ukanda wa Gaza na huu ni ushahidi wa ukweli usiweza kupingika nao ni udhaifu wa nchi hiyo."

Ayatullah Khamenei amezungumzia pia azimio la kuiwekea vikwazo Iran lililopasishwa na Baraza la Usalama na vitisho vya mara kwa mara vya kuishambulia kijeshi Jamhuri ya Kiislamu. Amesema: "Wanatoa matamshi ya kututaka tufikirie kwamba nyuma ya vitisho hivyo kuna hatari kubwa. Hata hivyo tunawajibika kujitayarisha kwa hali yoyote ile kwa ajili ya kulinda Mapinduzi ya Kiislamu na taifa azizi na lenye fahari la Iran, sawa vitisho hivyo viwe vya kweli au makelele matupu."

Kuhusu kadhia hiyo, Ayatullah Khamenei amesema kuwa njama nyingi zinazofanywa na Marekani ni za kisiasa na akaongeza kuwa katika fitina za mwaka jana Wamarekani waliingia katika medani haraka mno na kuwaunga mkono waziwazi viongozi wa fitina hizo; hata hivyo Mola Muweza, kuwa macho wananchi na kusimama kidete kwa taifa la Iran kulizima njama na mipango yao.

Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amewataka viongozi wote wa masuala ya siasa, uchumi, utamaduni na masuala ya kijamii kutilia maanani uhakika wa mambo ya ndani ya nje ya nchi na kutaamali utendaji wa maadui hapa nchini. Amesema hapana shaka kuwa taifa la Iran, Mapinduzi ya Kiislamu na Jamhuri ya Kiislamu itaibuka mshindi katika mpambano huo kama ilivyokuwa huko nyuma, kwani Mwenyezi Mungu Mtukufu amewaahidi wamchao kwamba watapata ushindi wa mwisho na ahadi ya Mola itatimia.

Ayatullah Ali Khamenei amesema kuwa imani, ucha-Mungu, amali na matendo mema hutayarisha uwanja mzuri wa kupata ushindi katika medani za kupambana na maadui wa Uislamu na Mapinduzi ya Kiislamu. Ameongeza kuwa mambo hayo yameyalinda Mapinduzi na kuyafanya yashinde mbele ya njama zote na hali hii itaendelea kuwa hivyo.

Mwishoni mwa hotuba yake, Amirijeshi Mkuu wa majeshi ya Iran amesema kuwa propaganda chafu zinazofanywa na maadui na vibaraka wao wa ndani dhidi ya Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ni dalili ya taathira kubwa ya jeshi hilo katika kudumisha harakati imara na ya fahari ya taifa la Iran. Amewausia pia wanachama wa jeshi hilo kuchunga nafsi zao na kuwajibika ipasavyo katika kutekeleza majukumu na kazi zo.

Amesema kuwa jeshi la Sepah ni familia moja kubwa, hai na yenye nishati. Vilevile amesisitiza juu ya udharura wa kuwapo ushirikiano kati ya sehemu mbalimbali za taasisi hiyo kubwa na akasema hata askari waliostaafu wa jeshi hilo wanahesabiwa kuwa ni wanachama wake.

Mwanzoni mwa mkutano huo mwakilishi wa Faqihi Mtawala katika Jeshi la Sepah Hujjatul Islam Walmuslimin Saidi amezungumzia harakati ya jeshi hilo katika misingi ya sheria na kanuni na akasema taratibu mpya za jeshi hilo zinatayarishwa.

Kamanda wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu Meja Jenerali Ja'fari pia ametoa ripoti fupi kuhusu mkutano wa 19 wa makamanda na viongozi wa jeshi la Sepah na kusema kuwa miongoni mwa ajenda kuu za mkutano huo ilikuwa ni pamoja na suala la kujitayarisha kwa hali yoyote, nafasi na mchango wa jeshi hilo katika mwongo wa nne wa Mapinduzi ya Kiislamu na njia za kupambana na vita laini.